Kamati ya Fedha, Uongozi na Mipango ya Halmashauri ya Wilaya ya Geita leo Januari 19, 2026, imefanya ziara ya kutembelea na kukagua utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo katika kata tofauti za halmashauri hiyo. Ziara hiyo imeongozwa na Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Geita, Mhe. Sylivester Kahesi, pamoja na Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri Lilla Kibuga, wakuu wa idara na wataalamu kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Geita. Kata zilizotembelewa ni Nyamigota, Ludete, Magenge na Lwamgasa.



Wajumbe wa Kamati ya fedha, uongozi na Mipango wakitembelea mradi ujenzi wa madarasa sita na matundu 12 ya vyoo vya shule ya msingi, pamoja na ujenzi wa madarasa mawili na matundu sita ya vyoo vya elimu ya awali katika Shule ya Msingi Iseni.
Katika kata ya Nyamigota, kamati ilikagua mradi wa ukamilishaji wa nyumba ya mtumishi aina ya 3-in-1 katika Kituo cha Afya Nyamigota, unaotekelezwa kwa kutumia fedha za mapato ya ndani. Viongozi wa kamati waliipongeza hatua iliyofikiwa katika ujenzi huo na kusisitiza umuhimu wa kukamilisha mradi kwa wakati. Diwani wa Kata ya Busanda, Mhe. Selemani Gamala, aliwahimiza mafundi na watendaji wa kata kuhakikisha kazi inamalizika kwa wakati na mafundi kulipwa stahiki zao bila kucheleweshwa. Naye Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri, Mhe. Sylivester Kahesi, aliwataka watendaji kuendelea kufanya kazi kwa bidii na kutoa taarifa mapema endapo kutajitokeza changamoto zozote katika utekelezaji wa mradi.


Nyumba ya mtumishi aina ya 3-in-1 katika Kituo cha Afya Nyamigota, Ikiwa katika hatua za Ukamilishaji.
Ziara iliendelea katika kata ya Ludete, ambapo kamati ilitembelea mradi wa ujenzi wa madarasa matatu pamoja na matundu sita ya vyoo katika Shule ya Msingi Mji Mwema. Mradi huo umetekslezwa kupitia Mfuko wa Bakaa na tayari umekamilika na kuanza kutumika. Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri aliipongeza jamii ya eneo hilo kwa usimamizi mzuri wa mradi na kusema kuwa hatua hiyo inaonesha matumizi sahihi ya fedha za umma kwa manufaa ya wananchi.


Mradi Ujenzi wa madarasa matatu pamoja na matundu sita ya vyoo katika Shule ya Msingi Mji Mwema
Katika kata ya Magenge, kamati ilikagua ujenzi wa ofisi ya kata unaotekelezwa kwa kutumia fedha za mapato ya ndani. Viongozi wa kamati walieleza kuridhishwa na maendeleo ya mradi huo na kusisitiza umuhimu wa kuumaliza kwa wakati bila kusuasua ili uweze kuanza kutoa huduma kwa wananchi.

Mardi wa ujenzi wa ofisi ya Kata unaotekelezwa kwa kutumia fedha za mapato ya ndani
Kadhalika, katika kata ya Lwamgasa, kamati ilitembelea ujenzi wa jengo la maabara pamoja na ujenzi wa jengo pacha la wodi ya wazazi na upasuaji, miradi inayotekelezwa kupitia ufadhili wa Benki ya Dunia. Kamati ilisisitiza umuhimu wa kuzingatia ratiba ya utekelezaji na kuhakikisha changamoto zote zinazojitokeza zinatatuliwa kwa haraka ili miradi hiyo ikamilike kwa wakati na kuwanufaisha wananchi.
Pia katika kata ya Lwamgasa, kamati ilitembelea ujenzi wa madarasa sita na matundu 12 ya vyoo vya shule ya msingi, pamoja na ujenzi wa madarasa mawili na matundu sita ya vyoo vya elimu ya awali katika Shule ya Msingi Iseni, miradi inayotekelezwa kupitia fedha za Bakaa. Akisoma taarifa ya mradi mbele ya kamati, Mkuu wa Shule ya Msingi Iseni, Paschal Sweke, alisema kuwa utekelezaji wa miradi hiyo utasaidia kupunguza msongamano wa wanafunzi madarasani, kupunguza michango ya maendeleo kwa wananchi na kusaidia kupunguza tatizo la utoro shuleni. Kamati iliipongeza jamii na uongozi wa shule kwa kazi nzuri na kuwataka walimu kuongeza bidii katika kufundisha ili matokeo ya kitaaluma yawiane na ubora wa miundombinu iliyopo.
Kwa ujumla, Kamati ya Fedha, Uongozi na Mipango ya Halmashauri ya Wilaya ya Geita imeeleza kuridhishwa na maendeleo ya miradi iliyotembelewa na kuhimiza watendaji na wadau wote kuendelea kusimamia kwa karibu utekelezaji wa miradi ya maendeleo ili ihitimishwe kwa wakati, kwa ubora unaotakiwa na kwa kuzingatia matumizi sahihi ya fedha za umma kwa manufaa ya wananchi wa Wilaya ya Geita.
Halmashauri ya Wilaya ya Geita
Anuani ya Posta: S.L.P 139 Geita
Simu: +225 282520061
Mobile:
Barua pepe: info@geitadc.go.tz
Hakimiliki@ Halmashauri ya wilaya ya Geita , Haki zote zimehifadhiwa